Monday, May 20

Waandishi wa habari ni wadau muhimu katika uhifadhi na utunzaji Mazingira

NA ABDI SULEIMAN, BAGAMOYO.

MKURUGENZI Mtendaji wa Chama Cha wa Wandishi wa Habari za Mazingira Tanzania (jET) John Chikomo, amesema waandishi wa habari ni wadau muhimu katika suala zima la kuelimisha umma wa watanzania juu ya suala la uhifadhi na utunzaji wa mazingira nchini.

Alisema waandishi wa habari hawako mbali na wadau wengine, kwani wanajukumu kubwa kwa kutumia vyombo vyao vya habari, kwani jamii iliyokubwa inapata taarifa za uhifadhi kwa haraka.  

Chikomo aliyaeleza hayo wakati akifungua mafunzo kwa waandishi wa habari 20 kutoka Tanzania bara na Visiwani, juu ya masuala mbali mbali ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira, ikiwa ni utekelezaji wa Mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasiji Unaotekelezwa na JET Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani.

“Jukumu la wanahabari ni kubwa kwa kutumia kalamu zao, vyombo vyao jamii iliyokubwa inaweza kupata taarifa kwa haraka sana, wapo watu wanajifunza kutokana na kusoma na kusikia taarifa nzuri za uhifadhi zile nzuri zinazofanyika,”alisema.

Alisema yapo maeneo watu wameshapata uwelewa na wakombele, katika suala zima la kuhakikisha uhifadhi na utunzaji wa mazingira, misitu na wanyamapori inazingatiwa.

Aidha alisema JET imekua ikitoa mafunzo tokea kuanzishwa kwao mwaka 1991 na asilimia 75 ya waandishi imeshapata mafunzo, na wataendelea kutoa mafunzo kila wanapopata miradi ili kuona waandishi wote wanapata mafunzo na kuandika kwa ufasa habari za utunzaji wa mazingira.

Nae Afisa uhifadhi kutoka wakala wa huduma za Misitu Tanzania (TFS) Ruben Magandi, aliwataka wananchi kuendelea kulinda maliasi zilizopo nchini, kwani serikali inawezesha kwa kutoa miche ili kurudisha uoto wa asili uliopotea.

Alisema serikali inatoa hadi miti ya matunda ili kusaidia kuongeza kipato kwa wananchi baada ya kupanda na mwisho wa siku wanapovuna.

Aidha alisema TFS inashirikiana na taasisi mbali mbali katika kutunza maliasili, pamoja na kuzuwia uharibifu wa mazao ya misitu kwa kushirikisha jamii.

Kwa upande wa shoroba alisema, TSF inahusika katika kulinda maliasili zilizopo kwenye shoroba mbali mbali, ili kuona mali asili hizo haziharibiwi.

“Katika kuhakikisha maliasili hazitoweki, juhudi zimeshafanyika ni kushirikiana na mashirika mengine, kushirikisha mikataba mengine ya kimataifa ambayo inalinda mimea iliohatarini kutoweka,”alisema.

Kwa upande wao waandishi wa habari za mazingira waliopatiwa mafunzo hayo, wamesema yamewasaidia sana kujua sharia, kanuni mbali mbali za uhifadhi wa mazingira na kujua athari za uharibufi kwa sasa.

Kwa Upande wake Mwandishi wa habari kutoka Gazeti la Uhuru Athnath Mkiramwini, alisema amejifunza jinsi ya kuripoti habari za mazingira hasa katika masuala ya uhifashi jinsi ya kuisaidia jamii kuondokana na matumizi mabaya ya uharibifu wa Mazingira.

“Jukumu langu mimi mwandishi wa habari ni kuelimisha jamii, jinsi gani tunaweza kusaidia kutunza mazingira yetu, ili baadhi ya maliasili ambazo ni tegemezi kwetu zisiweze kupotea,”alisema.

Nae Mwandishi wa habari Sidi Ngumia kutoka bloga ya Fullshangwe, alisema mafunzo yanayowaweka katika nafasi ya kuandika habari za masingira kwa ufasaha sana.

Alisema tatizo la uharibifu wa mazingira linamuhusi kila mtu, wadau wa mazingira na jamii kila mtnu anapaswa kutia nguvu zake ili kuhakikisha mazingira yanaokolewa.

Chama cha waandishi wa habari za Mazingira Tanzania (JET) kipo katika awamu ya tatu ya utekelezaji wa mradi wa USAID Tuhifadhi Maliasi, mradi ambao umekua ukitoa mafunzo mbali mbali kwa waandishi wa habari Tanzania juu ya masuala ya uhifadhi wa mazingira na Wanyamapori.

MWISHO 

Abdi Juma Suleiman

Journalist/Photographer

Zanzibarleo newspaper/Habari Portal.blog
Chake Chake -Pemba
+255774565947 or +255718968355